Blogger Widgets FURSA KWA VIJANA WOTE TUPAMBANE KWA KILA NJIA ILI MRADI TUWEZE KUEPUKA HUU UMASKINI TANZANI NA AMIN KILA ATAFUTAYE KWA NIA HUPATA MAANA ATA MAANDIKO HUSEMA PENYE NIA PANA NJIA

Thursday, September 11, 2014

KUFANIKIWA KIHALALI KUNALETA HESHIMA



  • Written by  Tupambane Blog
  • Email
  • Tuma Maoni
  • Share on facebook Share on google_plusone_share Share on twitter 
karia_a0262.png

Na, Thommy kundy Moshi
Nyakati za sasa watu wengi wapo bize kuyasaka mafanikio ya kiuchumi kila mahali. Maisha ya sasa yamekuwa na misukumo na mibinyo mikubwa. Kila kitu kwa sasa hakiendi ama kufanikiwa pasipo mtu kuwa na uchumi imara, ama kwa kifupi tuseme fedha.
Fedha imekuwa ndio "habari ya mjini", inatafutwa kwa udi na uvumba. Suala la watu kuhangaika na maisha [kutafuta fedha] ni jambo jema; lakini namna gani (kwa njia gani) watu wanahangaikia hayo maisha ndio jambo lililoniinua kuandika makala haya.
Nimepata kufuatilia habari ya Wamarekani tisa marafiki walioshibana ambao walikuwa matajiri kupindukia lakini utajiri wao waliupata kwa njia za ujanja-ujanja. Inaelezwa kwamba mwaka 1923 walikutana katika hoteli maarufu sana ya Hedge-Water; kwa lengo la kuunganisha ukwasi wao ili wawe na nguvu na sauti zaidi katika uchumi wa taifa lao na dunia kwa ujumla.(P.T)
Ukwasi wao [kwa pamoja] ulikuwa ni mkubwa kuliko hazina ya serikali ya Marekani kwa wakati huo. Walipendwa na kutamaniwa na watu wengi katika mataifa mbalimbali lakini ilikuwepo siri kubwa sana nyuma ya mafanikio yao. Licha ya kwamba hawa walikuwa ndio wakopeshaji na wafadhili wakubwa wa kifedha duniani lakini miisho yao ilikuwa ni mibaya na yenye aibu.
Howard Hopson alikuwa mmilikiwa kampuni kubwa kabisa ya gesi, iitwayo Associated Gas and Electric Co. Hadi kufika mwaka 1925 alikuwa na zaidi ya makampuni 250 yaliyotawanyika kuanzia Ufilipino, Marekani, Kanada na duniani pote! Mwisho wake ulikuwa ni kufilisika na kufungwa jela baada ya kufanya udanganyifu kwa wanahisa unaokadiriwa kufikia dola milioni 20.
Charles Swart alikuwa rais wa kampuni kubwa kuliko zote ya masuala ya chuma. Mwisho wa huyu bwana ulikuwa ni ufukara baada ya kuishi kwa takribani miaka mitano kwa madeni. Mwingine ni Samwel Insole aliyekuwa rais wa kampuni ya kihuduma nae alifariki kifo cha aibu akiwa uhamishoni nchi ya ugenini. Yupo pia Arthur Carltonn aliyekuwa mfanyabiashara mashuhuri katika mazao ya ngano nae alifariki akiwa kafilisika yeye na kampuni yake.
Richard Whitney yeye alikuwa rais wa soko la hisa la NewYork (NewYork Stock Exchange). Whitney alijulikana sana kwa maisha ya anasa na alikuja kufia gerezani baada ya kupatikana na hatia ya kuiba rasilimali za NSE pamoja na kutoka kwenye benki ya Morgan akishirikiana na kaka yake. Alikuwepo pia Jesse Luminal aliyemiliki kiwanda kikubwa kabisa cha bia pale Wall Street baada ya mambo kumuwea magumu aliishia kujinyonga.
Albert Force nae alikuwa waziri mwenye ushawishi mkubwa sana katika baraza la mawaziri yeye alifia gerezani kwa kosa la udanganyifu. Lesser Frazer alikuwa ni rais wa benki ya makazi ya kimataifa nae aliishia kujinyonga. Ivan Krugar aliyekuwa mmiliki wa kampuni kubwa kabisa nae yalipomfika shingoni aliamua kujinyonga.
Tupo katika jamii ambayo inatukuza na kuufurahia fedha zisizo halali; leo hii mtu anaelipwa laki sita kwa mwezi akiwa hana biashara yeyeote zaidi ya mshahara wake; ni kawaida kumkuta akiendesha gari la milioni mia moja, akiishi kwenye nyumba yake binafsi ya milioni mia mbili. Lakini wanaomzunguka wengi utastaajabia kuona wakimsifu na kumuona kama mjanja na mtafutaji!
Akili za wengi sasa zimejikita katika kuvizia fedha za mikato-mikato pasipo kujali nani anaumia. Watu wanaiba madawa hospitalini watu wanakufa halafu wakifanikiwa tunasema wamebarikiwa! Watu wakiingia makazini wanatafuta mipenyo haramu ili kutajirika na "kuyafurahia maisha". Bahati mbaya ni kwamba hauwezi kuwa na amani [ya ndani] ikiwa mafanikio yako kifedha yamepatikana kwa njia zisizo halali.
Maandiko matakatifu yanatuasa kwamba tunapoishi duniani uovu hauwezi kukoma. Katika uovu huo kuna watu wengi watataka kufanikiwa kwa njia za mikato mikato na ujanja ujanja; ndio maana tukaambiwa kuwa usiwahusudu(usiwatamani) waovu(wenye kutumia hila) wanapofanikiwa.
Mtu anauza unga, mtu anafisadi kazini, anafanya magendo; na sote tunakuwa tukijua; kisha anajenga maghorofa anamiliki mapesa fedha na utitiri wa mali; halafu unatamani umfikie? la hasha! Tunaambiwa tusiwatamani kwa sababu miisho yao ni mibaya. Laana ya kupata mali ama mafanikio kwa hila haimuachi mtu kirahisi; isipopiga afya yake itapiga familia yake, isipopiga familia yake itaua jina lake; hayo yasipotokea laana hiyo itapenya mpaka kwenye vizazi vyake
Leo hii ukiongea suala la usafi wa kimaadili(hasa katika fedha) watu wengi watakushangaa. Watakushangaa kwa sababu suala la "kukwapua" limekua la kawaida sana. Hata hivyo, ukitaka kuwa wa tofauti ni lazima ujizoeze kufanya mambo ya tofauti. Kama wengine wanaiba, huna sababu ya kuiba kwa sababu madhara ya wizi, udokozi na ufisadi wako hayatakuwa ya umma bali ya peke yako wewe mwenyewe.
Wapo mamia ya wafanyabiashara ambao wanafanikiwa kwa njia ya magendo, kwa njia ya kuiibia serikali kodi, utapeli na mikato mikato. Watu wanafurahia mali za kitambo lakini mafanikio yanayopatikana kwa namna hii mara nyingi huwa hayana mwisho mzuri. Unaweza 'ku-win' wewe lakini ukakiachia kizazi chako matatizo makubwa usivyodhania.
Ni vema kujifunza kutafuta mafanikio na utajiri wa haki. Kwa mujibu wa maandiko matakatifu[Biblia], utajiri na mafanikio ya haki yana sifa kubwa tatu. Kwanza yanakuwa ya kizazi na kizazi, pili hayaambatani na majuto na tatu yana ulinzi wa kuaminika. Vile vile maandiko yanatutahadharisha kwamba mafanikio na utajiri vilivyopatikana kwa pupa hutoweka ghafla
Kuna umaana gani mtu kuwa na mali leo halafu watoto wako wakaishia kuwa ombaomba ama vizazi vyako vikakosa cha kurithi na kukukumbuka? Kuna haja gani mtu kuwa na utajiri mkubwa halafu uishie kuwa na mikasa itakayokuletea majuto? Fikiria mfanyabiashara anaefanya biashara kwa kukwepa kodi, siku akikumbana na mkono wa dola akafalisiwa bila shaka ataishia kwenye majuto makubwa.
Watu wanapata mafanikio na utajiri kwa njia ambazo zinahatarisha hadi afya zao (misongo, mawazo, misukosuko); mwisho wanajikuta wakipata presha, magonjwa ya moyo na madhara mengine yatokanayo na kukosekana msawazo wa kimwili. Sasa kuna haja gani ya kuwa na mafanikio na mali ambavyo mwisho wa siku vitakuja kutumika kugharimia kutibu afya yako?
Utajiri na mali zinazopatikana kwa hila ama ujanjaujanja hazidumu, hazina uhuru nakamwe hazina heshima pia.Namna zlivyopatikana ni siri ya mhusika.Mtu mwenye mafanikio ya jinsi hii hayuko huru hawezi kueleza kwa uwazi chimbuko la utajiri wake.Na ikilazimu basi kufanya hivyo atasema uongo tu!Kweli utawadanganya wengine lakini dhamira yako ya ndani haitaacha kukusuta,hamna heshima hapo!
Wanasema pesa inaleta heshima, pesa sabuni ya roho; hata hivyohilo linategemeana umezipataje.Hebu fikiria mtu anayepata pesa na mali kwa njia ya utapeli, dhuluma kwa wanyonge,kuudhalilisha mwili wake,kukatisha maisha ya watu wasio na hatia kwa kumwaga damu zao ili mradi tu ufanikiwe; Je hiyo ndio heshima yenyewe? Ama sabuni gani inayotokana na ubaya wa namna hii?

No comments:

Post a Comment

TUPAMBANE BLOG