Blogger Widgets FURSA KWA VIJANA WOTE TUPAMBANE KWA KILA NJIA ILI MRADI TUWEZE KUEPUKA HUU UMASKINI TANZANI NA AMIN KILA ATAFUTAYE KWA NIA HUPATA MAANA ATA MAANDIKO HUSEMA PENYE NIA PANA NJIA

Thursday, October 16, 2014

NAMNA MWANAMKE ANAVYOWEZA KUTUMIA NAFASI ZAKE KUBADILISHA MAISHA YA NDOA YAKE


Na: Patrick Sanga
Maada: Nafasi ya Msaidizi, Mshauri na Mleta kibali  
Ili kusoma sehemu ya kwanza bonyeza link hii http://sanga.wordpress.com/2014/10/16/namna-mwanamke-anavyoweza-kutumia-nafasi-zake-kubadilisha-maisha-ya-ndoa-yake/
Mpenzi msomaji, Mungu akubariki kwa kufuatilia mfululizo wa somo hili. Ni imani na maombi yangu kwamba masomo haya yatafanyika msaada kwenye maisha yako na ndoa yako kwa ujumla. Katika sehemu hii ya pili nitaandika kuhusu nafasi tatu ambazo ni nafasi ya Mwanamke kama Msaidizi, Mshauri na Mleta kibali.
Mwanamke kama Msaidizi
Mwanzo 2:18 ‘BWANA Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye’.  Ukisoma mstari huu katika toleo la GNB Biblia inasema ‘Then the LORD God said, “It is not good for the man to live alone. I will make a suitable companion to help him.” Biblia inatueleza kwamba Adam ndiye aliyetangulia kwanza kudhihirishwa kabla ya Mwanamke. Kabla ya Hawa kuletwa, Mungu alimpa Adam majukumu mengi ambayo alipaswa kuyatekeleza.
Katika kutekeleza majukumu yake Adam aliona kwamba amepungukiwa mwenza wa kufafanana naye na ndani yake akatamani angepata mtu wa kuwa naye karibu kwa kila afanyalo. Ukweli huu tunaupata tukisoma Mwanzo 2:20 kwamba ‘Adamu akawapa majina yao kila mnyama wa kufugwa, na ndege wa angani, na kila mnyama wa mwituni; lakini hakuonekana wa kumsaidia Adamu aliyefanana naye. Naam kutokana na upweke wa Adam ndipo Mungu akamfanya Hawa mkewe kama msaidizi. Kitendo cha Mungu kumfanya mwanamke kama msaidizi ni ishara kwamba Mungu alijua kuwa Adam hawezi kuwa na ufanisi mzuri katika kutekeleza majukumu (Kusudi) aliyopewa bila mwenza wa kufanana naye.
Maandiko yanasema kwamba ‘Maana mwanaume hakutoka katika mwanamke, bali mwanamke katika mwanaume. Wala mwanaume hakuumbwa kwa ajili ya mwanamke, bali mwanamke kwa ajili ya mwanaume’ (1Wakorinto 11:8-9).  Ile kwamba mwanamke aliumbwa kutoka kwa mwanaume na kwa ajili ya mwanaume ni kuonyesha kwamba wajibu au nafasi mojawapo ya mwanamke ni kuwa msaidizi wa mumewe. Hata hivyo neno msaidizi halipaswi kutafsiriwa vibaya na kuonyesha kwamba mwanamke hana thamani.
Mwanamke ni msaidizi wa mume katika kulitumikia kusudi la Mungu isipokuwa kinacho watofautisha ni utendaji wao tu. Mume hapaswi kumdharau mkewe wala mke kumdharau mumewe kwa kuwa mume si mume bila mke na mke si mke bila mume, wao ni mwili mmoja, kusudi lao ni moja na BWANA wao ni mmoja.   Maandiko yafuatayo yanaonyesha baadhi ya mambo ambayo mwanamke anapokuwa katika nafasi ya Msaidizi anapaswa kuyafanya;
Tito 2:4 inasema ‘Ili wawatie wanawake vijana akili, wawapende waume zao, na kuwapenda watoto wao, na kuwa wenye kiasi, kuwa safi, kufanya kazi nyumbani mwao, kuwa wema, kuwatii waume zao wenyewe; ili neno la Mungu lisitukanwe’.
1 Timotheo 5: 14 ‘Basi napenda wajane, ambao si wazee, waolewe, wazae watoto, wawe na madaraka ya nyumbani; ili wasimpe adui nafasi ya kulaumu’. Ukisoma pia katika 1 Wakorinto7:4a kwa habari ya tendo la ndoa Biblia inasema ‘Mke hana amri juu ya mwili wake…’ na mstari wa 5a unasema’ Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda…, Naam hii ina maana kama mke ataweka amri kwa habari ya tendo la ndoa kwa mumewe ajue kabisa ameshindwa kumsaidia mumewe na kuna hatari ya kuanguka kwenye zinaa. Naam Mungu anataka akina mama walioko kwenye ndoa wajifunze kuwasaida waume zao wasiingie kwenye zinaa.
Naam hata sasa ni muhimu sana wewe mama ukajua Mungu amewaunganisha ili kufanya nini hapa duniani kwa ajili ya ufalme wake. Changamoto kubwa iliyipo leo ni kwamba wanandoa wengi wameingia kwenye ndoa kwa sababu ni desturi ya wanadamu kuoa na kuolewa. Wengi wameshindwa kuunganisaha suala la kuoa au kuolewa na kumtumikia Mungu kupitia ndoa yao. Mungu anapokuunganisha na mumeo maana yake anakupeleka kwenye wajibu wa kuwa msaidizi kwa mumeo. Naam hakikisha kwamba unafanyika msaada kwa mumeo kwa namna ambayo kile ambacho mnajua kwamba Mungu amewapa kukifanya hapa duniani kinafanikiwa. Zaidi unaweza soma Mithali 31:10-31 ili kuongeza ufahamu zaidi kuhusu nafasi ya mwanamke kama Msaidizi.
Mwanamke kama Mshauri
Katika hali ya kawaida watu wengi hutafsiri mshauri kuwa msiaidizi. Kwa kuzingatia dhana ya nafasi katika ulimwengu wa roho imenilazimu kutenganisha ili kukuonyesha umuhimu wa nafasi ya mwanamke kama Mshauri. Biblia katika Mithali 31:26 inasema ‘Hufumbua kinywa chake kwa hekima, Na sheria ya wema i katika ulimi wake’.
Naam andiko hili linatupa kujua kwamba Mke ndiye mshauri mkuu wa mumewe. Siri moja ya mwanamke kuwa mshauri mzuri ni kuwa na ufahamu wa kutosha wa neno la Mungu. Hivyo kama Mke hana hekima itokanayo na neno la Mungu kwa wingi ndani yake, hawezi kuwa mshauri mzuri. Ushauri unategemea nguvu za ufahamu alizonazo Mwanamke, kadri anavyokuwa na ufahamu wa kutosha wa neno ndivyo anavyokuwa kwenye nafasi ya kutoa ushauri bora kwa mumewe.

Biblia katika kitabu cha Mithali 8: 14-16 inasema ‘Shauri ni langu, na maarifa yaliyo sahihi; Mimi ni ufahamu na mimi nina nguvu. Kwa masada wangu wafalme humiliki, Na wakuu wanahukumu haki. Kwa msaada wangu wakuu hutawala, Na waungwana, naam, waamuzi wote wa dunia’. Fahamu kwamba hekima ndani yako mama itakupa maarifa na ufahamu wa kumshauri mumeo ili kufanya maamuzi sahihi katika kila atendalo. Hekima ni sawasawa na   shauri/maarifa/ufahamu/nguvu. Ukiona kiongozi yoyote anatawala/anaongoza watu vizuri ujue washauri wake wanamshauri vizuri au ujue ana wahsauri wazuri. Vivyo hivyo mwanaume anafanya kazi zake vema na kufanikiwa katika yale atendayo ujue nyuma yake kuna mwanamke mwenye nguvu za ufahamu anayemshauri vema.
Naam chanagmoto au matatizo mengi yaliyopo kwenye ndoa leo ni matokeo ya akina mama kukosa hekima itokanayo na neno la Mungu ya kuwashauri waume zao. Wengi wanategemea akili zao, au ushauri wa rafiki zao nk. katika kuangalia ndoa zao na mambo yao yaendaje. Kutegemea ushauri wa watu wengine bila wewe mwenyewe mama kutafuta hekima itokanyo na Mungu kwanza inaweza kukufikisha kupata ushauri wa kipepo kama ilivyomtokea Hawa pale Bustanini. Kumbuka Mshauri ni mtoa taarifa, mtoa pendekezo juu ya nini mume wake aweza fanya au kutofanya.
Mwanamke kama mleta kibali.
Hii ni nafasi ya ajabu sana ambayo Mungu amempa mwanamke. Mwanamke anapokuwa kwenye hii nafasi mambo matatu yanafanyika; 1) Mume anaingia kwenye ngazi ya kushirikishwa siri/mambo/majukumu mengi kutoka kwa BWANA. 2) Kukubalika kwa mume wake katika jamiii/kazi/kanisa nk kunaongezeka 3) Na mwisho maombi ya mume wake yanasikilizwa. Mambo haya yanathibitishwa na Biblia katika  Mithali 18:22 inayosema ‘Apataye mke apata kitu chema; Naye ajipatia kibali kwa BWANA’, pia   Mithali 31: 23 inayosema ‘Mume wake hujulikana malangoni; Aketipo pamoja na wazee wa nchi’
Zaidi kwa habari ya maombi ya mume kusikilizwa au kutokusikilizwa Biblia katika      1 Petro 3:7 inasema ‘Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe’. Naam hii ni ishara kwamba mke anaweza kusababisha maombi ya mumewe yakasikilizwa au yasisikilzwe. Unaweza ukafikiri hili andiko linawahusu akina baba pekee, lakini ukilitafakari kwa upana utagundua kwamba linawahusu akina mama pia ili wajue kwamba kuwa mke ni nafasi ambayo inaweza kuzuia maombi/baraka/majibu au kukwamisha mafanikio ya waume zao kama hawatukuwa makini katika kuwasaidia waume zao kuishi nao kwa akili.
Si wengi wanaojua kwamba kuna maombi mengi ya familia/waume zao hayajibiwi kwa sababu maombi ya mume ambaye ndiye kichwa hayasikilizwi na Mungu. Na chanzo cha kutokusikilizwa ni kuharibika kwa uhusiano kati ya mume na ‘mleta kibali’ wake yaani mke. Hivyo wewe mama mwenye ufahamu huu jifunze kwenda mbele za Mungu na kuomba toba kwa ajili ya mumeo mara kwa mara. Kwa sababu kuna vitu au maamuzi anayoweza kufanya nay eye akaona yuko sahihi lakini kumbe ni uamuzi ambao unajenga ukuta kati ya maombi yake na Mungu wako.

Hakikisha unasimama vema kwenye hii nafasi ili Mungu alete uponyaji kwa mume wako na maombi yake yaweze kusikilizwa. Naam simama kwenye nafasi yako ili kumjengea mazingira mazuri mumeo ya kuishi na wewe, ndivyo na maombi yake yatakavyosikilizwa, ndivyo atakavyopata kibali mbele za BWANA, naam atakuwa mume bora katika jamii na kufanikiwa katika kila atendalo.
Tamati endapo mwanamke atakaa vizuri kwenye nafasi hizi haijalishi mume wake ni mgumu kiasi gani, mama akizungumza kwa maana ya maonyo au ushauri lazima mwanaume asikilize au kufuata kile ambacho msaidizi, mlinzi, mleta kibali wake nk anamweleza, na kama akikataa uharibifu ni haki yake. Mungu ameweka sauti ndani ya mwanamke ambayo inaweza kuleta uponyaji kwa mumewe endapo mwanamke atakaa vizuri kwenye hizi nafasi.
Ubarikiwe, tutaendelea na sehemu ya tatu…

No comments:

Post a Comment

TUPAMBANE BLOG