Na Greyson Mwase, Mbeya
Maafisa Mazingira katika wilaya zilizopo katika mikoa ya Iringa na Mbeya wametakiwa kuacha kuwabembeleza wawekezaji wasiozingatia sheria za uhifadhi wa mazingira.
Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Mbeya , Constantine Mushi wakati akifungua mafunzo ya siku tano yaliyoshirikisha maafisa mazingira kutoka katika wilaya 14 za mikoa ya Iringa na Mbeya ikiwa ni pamoja na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) na Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali.
Mushi alisema kuwa wapo baadhi ya wawekezaji katika sekta za madini na nishati wasiozingatia sheria ya mazingira ya mwaka 2004 inayotaka shughuli yoyote ya maendeleo kuendana na uhifadhi wa mazingira na hivyo kuchangia uharibifu mkubwa wa mazingira.
Alisema kuwa maafisa mazingira wanatakiwa kusimamia sheria za mazingira kwa kuhakikisha kuwa zinafuatwa ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua kali wawekezaji wasiozingatia sheria hizo.
Alisema kuwa katika sekta ya nishati kuna shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi unaoendelea sehemu mbalimbali nchini katika nchi kavu, kwenye ukanda wa bahari, katika maji ya kina kirefu baharini (deep sea) na kwenye maziwa na kusisitiza kuwa hii ni changamoto kwa maafisa mazingira katika kutoa ushauri na kuhakikisha kuwa binadamu na viumbe wengine hai hawaathiriwi na uwekezaji huu.
Alieleza kuwa uwekezaji katika sekta ya nishati ni mkubwa sana kwani nishati ya umeme ina mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi, hivyo suala la mazingira linatakiwa lizingatiwe ili kuhakikisha kuwa wananchi na viumbe wengine hawaathiriwi na uwekezaji huu.
Aliongeza kuwa uwekezaji katika sekta ya madini katika miaka ya karibuni umekua kwa kasi kubwa sana lengo lake likiwa ni kuleta maendeleo na kusisitiza kuwa shughuli za uchimbaji madini zisipofuata kanuni na sheria za mazingira zinaweza kuacha nchi ikiwa jangwa na kuathiri mabadiliko ya tabia nchi.
“Ni jukumu letu sote kuhakikisha kuwa shughuli zote za maendeleo zinafanyika bila kuleta athari kubwa katika mazingira yetu kwa kusimamia sheria na kanuni za mazingira pasipokuwa na upendeleo,” alisisitiza Mushi.
Alisema kuwa kuzingatia hitaji la sheria ya mazingira, Wizara ya Nishati na Madini imeandaa mpango kazi wa mazingira wa sekta za nishati na madini (sector environmental action plan) ambao utekelezaji wake utaenda hadi katika ngazi ya wilaya.
Wakati huo huo Mkuu wa Kitengo cha Mazingira, Wizara ya Nishati na Madini Mhandisi Gideon Kasege alisema lengo la mafunzo hayo ni kuwashirikisha maafisa mazingira mpango kazi wa mazingira wa sekta za nishati na madini wa Wizara, kuwapa elimu ya mazingira na kupata michango yao ili kuwa na mkakati wa pamoja wa kuhakikisha kuwa sheria na kanuni za mazingira zinafuatwa.
Mhandisi Kasege alisema kuwa awamu ya kwanza ya mafunzo hayo yalishirikisha mikoa ya Kanda ya Pwani kama vile Dar es Salaam, Tanga, Mtwara, Morogoro na Kilimanjaro, awamu ya pili katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ambayo ni Mwanza, Simiyu, Geita, Mara, Kigoma na Tabora na kuongeza kuwa awamu ya tatu inahusisha mikoa ya Iringa na Mbeya.
Alisema kuwa mafunzo haya ni endelevu na kusisitiza kuwa mikoa iliyobaki kama Katavi, Rukwa, Njombe, Ruvuma, Dodoma, Arusha ambayo bado haijafikiwa itashirikishwa katika awamu ya nne.
Alieleza kuwa mpango huo wa miaka mitano ulioanza mwaka 2011 unatarajiwa kukamilika mwaka 2016.
Naye Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kusini Magharibi Wilfred Machumu alisema kuwa mafunzo hayo yatatumika kama fursa ya maafisa mazingira kubadilishana uzoefu na changamoto katika usimamizi wa mazingira na hatimaye kupata mkakati wa pamoja wa kuboresha usimamizi wa mazingira.
No comments:
Post a Comment