Jinsi ya kutunza miti ya Michungwa
Miti ya michungwa inahitaji uangalizi wa hali ya juu, jambo ambalo wakulima wengi ama hawalijui ama hawatilii maanani. Miti hii hupandwa kwa mbegu za milimao ya kawaida (rough lemon) ambayo hutumika kama mti mama wa mchungwa halafu inaungwa/bebeshwa kwa kutumia vikonyo maalumu vya michungwa.
Miti hii inahitaji ukaguzi wa mara kwa mara ili kupunguza matawi yanayokuwa bila mpangilio kwani matawi haya huzuia mti kupata hewa kwenye shina.
Matawi haya ni pamoja na:
- Matawi yenye magonjwa, matawi haya huondolewa ili kuzuia ugonjwa usienee katika matawi ama kwenda kwenye mimea mingine.
- Matawi yaliyokufa au yaliyokauka huondolewa ili kuruhusu matawi mapya kuchipua.
- Matawi makubwa kuliko mengine na yanayoenda juu zaidi, huwa makubwa sana na hivyo kunyonya maji mengi ya mmea. Matawi haya yanaweza kutoa machungwa lakini machungwa yake huwa hayana maji kwani maji mengi hunyonywa na tawi.
- Matawi yanayoota kuelekea ndani/katikati ya mti, huzuia shina kupata hewa ya kutosha hivyo husababisha ugonjwa wa ukungu na wadudu kwa mmea.
- Matawi madogo madogo yanayoota katika tawi moja, huondolewa kwani yanasababisha mmea kuwa kama kichaka ambapo hewa na mwanga havifiki kirahisi kwenye shina.
Kupunguza matawi yasiyofaa katika mti (pruning) huongeza uhai wa mti na kuongeza uzalishaji kwa asilimia themanini ( 80%) na kupunguza magonjwa kwa asilimia hamsini ( 50% ). Zoezi hili la kupunguza matawi linashauriwa lifanyike mara baada ya kuvuna ili kuuandaa mti kwa msimu mpya wa uzalishaji.
Vitendea kazi vya kupunguzia matawi haya ni pamoja na mkasi maalumu wa kukatia matawi madogo na msumeno wa kupunguzia matawi makubwa.
Epuka kutumia panga kwani linaacha mpasuko kwenye kipande cha tawi linalobaki na kusababisha ugonjwa wa Gumosisi yaani mti kutoa kitu kama gundi katika eneo lenye mpasuko.
No comments:
Post a Comment