Mwenyekiti
wa Serikali ya Mtaa wa Shamariwa ‘A’, Kata ya Igoma, Wilaya ya
Nyamagana, jijini Mwanza, Julias Makoye (CCM), amekutwa amejinyonga juu
ya mti ulio jirani na nyumba yake usiku wa jana.
Makoye
aliyetangazwa mshindi wa kiti hicho katika uchaguzi wa serikali za
mitaa uliofanyika Desemba 14, mwaka jana, ameuongoza mtaa huo kwa awamu
ya pili baada ya kuongoza miaka mitano iliyopita.
Akizungumza
jana nyumbani kwake, mke wa marehemu, Ivona Polikalapo, alisema saa 10
juzi jioni alimsikia mumewe akiongea na mtu kwenye simu yake ya mkononi
na kumsisitiza anahitaji mzigo wake wote.
“Jana
(juzi) saa 10 jioni nilimsikia mume wangu akiongea na mtu katika simu
na kutaka alipwe mzigo wake wote kutokana na kukaa muda mrefu, lakini
aliyekuwa akizungumza naye sikumfahamu ni nani,” alisema Polikalapo.
Aidha,
alisema ilipofika saa 10 alfajiri ya jana, mbwa wao walisikika
wakibweka kwa muda mrefu hali iliyomfanya marehemu atoke nje kuangalia
kilichopo katika banda lao la mifugo huku (mke) akiendelea kuandaa
chakula cha mifugo hao.
“Baada
ya mume wangu kuamka na kwenda kuangalia kilichopo nje, hakuweza
kurejea ndani hadi pale nilipotoka kwenda kumwaga uchafu shimoni
nikashangaa baada ya kumuona ananing’inia juu ya mti…nilipojaribu
kumuita hakuitika,” alisema.
Hata
hivyo, mama huyo anasema haamini kama mume wake amejinyonga bali
kanyongwa kutokana na mti aliojitundika kutoonekana kuwapo na jiwe la
‘sapoti’ ili kutekeleza azma yake hiyo.
Mashuhuda wa tukio hilo, Joseph Okala, alisema mwenyekiti huyo alikutwa akiwa amening’inia katika mti akiwa ameshakata roho.
“Baada
ya kushuhudia hilo, watu walijaa eneo la tukio na kumuona mwenyekiti
wao Makoye akiwa ananing’inia kwenye mti uliopo mbele ya nyumba yake
lakini cha kushangaza haionyeshi kama alipanda juu kwani kamba ilikuwa
imeshika sehemu za masikio na kidevu tu,” alisema Okala.
Hata
hivyo, kaimu kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza, Japhet Lusingu,
alithibitisha kuwapo na tukio hilo, akidai Makoye alijinyonga huku
chanzo chake hakijafahamika.
No comments:
Post a Comment