Albert Sanga, Iringa.
Wiki hii
sikupanga kuandika makala hii. Nimeamua kuiandika kufuatia mazungumzo
niliyofanya na bwana mmoja ambae alijitambulisha kuwa ni "msomaji mgeni"
katika safu yangu hii. Aliponipigia simu alianzia mbali kweli lakini
pointi yake mwishoni akaniuliza, "Katika wagombea Urais waliotangaza na
kuonesha nia unamuunga mkono yupi ama unafikiri nani anafaa?"
Kwa
haraka haraka nikamwambia "Nitamuunga mkono na ikibidi kumsaidia mgombea
yeyote katika waliokwisha kujitokeza ama watakaojitokea; kwa sharti
moja kubwa; mgombea husika awe ni kiongozi mwenye maono na roho ya
kijasiriamali".
Msomaji
huyu mgeni, akang'ang'ana nimtajie jina(la mgombea ninaeoa ana hayo
maono na roho ya kijasiriamali), nikamjibu, "kichwani kwangu hakuna jina
isipokuwa kuna sifa na nikamtajia hizo sifa". Hakuridhika na majibu
yangu. Hata hivyo nikamwambia, "Hata kama hujaridhika ni lazima utambue
kuwa ninasimamia kile ninachokiamini"
Harakati
za Urais, ubunge na udiwani naona zimepamba moto karibu kila kona
nchini. Ukifuatilia kwa umakini hata sasa katika nchi hii,{utagundua
kuwa} uadilifu wa kiongozi unapimwa kwa kuangalia kiwango chake cha
umasikini. Kiongozi akionekana ana mali chache inahesabika kuwa ndie
mwadilifu, na mwenye mali nyingi anaonekana kuwa sio muadilifu.(T.K)
Kuna
maswali huwa tunasahau kuuliza linapokuja suala la kuwatathmini viongozi
wetu. Mosi ikiwa kiongozi analeta 'swaga' za kutaka kujionesha ni
masikini (ama wa kawaida), anatakiwa atueleze mambo mawili. Kwanza, ni
kwa nini amekuwa masikini katika nchi yenye utajiri mkubwa namna hii?
Kama yeye
anaetafutakutuongoza ameshindwa kukabiliana na umasikini,
atawezajekutuongoza sisi masikini kuufikia utajiri. Kuongoza ni kuonesha
njia, inawezekanaje mtu kutuonesha njia ya kwenda mahali ambako "eti"
anasema hakujui, hajawahi kufika na hana mpango wa kufika! Ndio,
kiongozi anaetuletea taswira ya kujifanya masikini ama wa kawaida
anawezaje kutufikisha kwenye mafanikio na utajiri?
Kwa nini
amekuwa wa kawaida katika nchi ambayo ni nzuri zaidi ya ukawaida? Ikiwa
kiongozi anaetafuta Urais amewahi kuwa mbunge ama waziri ni dhahiri
kwamba kuna mamilioni tulikuwa tukimlipa kupitia kodi zetu. Akisema hana
mali za maana itabidi atueleze ni akili gani alikuwa anaitumia
kujisimamia katika eneo la fedha?
Lakini
tukikukuta wewe mtafuta madaraka una mali za kupindukia ambazo huenda tu
na mashaka nazo; tutahitaji utupe maelezo ya kina namna ulivyozipata.
Hii itatusaidia kwa namna mbili. Kwanza tujiridhishe ikiwa ni mali
halali na pili ikiwa ni halali basi itatuhamasisha na sisi wananchi
unaotaka kutuongoza kufuata nyayo zako. Kwa maana chuma hunoa chuma,
kiongozi tajiri atazalisha wananchi matajiri na kiongozi masikini
atazalisha wananchi masikini.
Nafahamu
wazi kuwa, wagombea wengi wanaifahamu mitazamo ya sisi watanzania tulio
wengi; ambapo tunapenda na kufurahia viongozi masikini. Kwa hiyo
wagombea wengi hutaka kijionesha mbele ya wapiga kura ya kwamba wao
hawana mali, ni masikini, ni watu wa kawaida. Kinachofanyika ni kwamba
huficha kwa makusudi utajiri wanaomiliki. Mtu anaetuficha mali zake ni
rahisi kutuibia tumpapo madaraka.
Sifa ya
mjasiriamali ni kujilipa mwishoni. Mjasiriamali daima anatanguliza
maslahi ya biashara mbele. Tunamtaka Rais na wabunge ambao wataiendesha
serikali kiujasiriamali. Fedha ya kodi ikikusanywa mtazamo wa
kijasiriamali utataka zianze shughuli za maendeleo ndipo kufuatie kujaza
matumbo.
Viongozi
wanaoanza kukumbuka posho na masurufu yao halafu zinazobaki ndizo
wanaangalia kujenga matundu ya vyoo mashuleni; hawa bado hawaifai nchi
kama hii. Bila kuwa na viongozi waliofurika roho ya ujasiriamali nchi
hii itabaki masikini mpaka mwisho wa dunia! Ieleweke kwamba hapa
siongelei kiwango cha mali ama biashara wanazopaswa kumiliki hao
viongozi bali naongelea mtazamo wa kijasiriamali.
Viongozi
wenye mtazamo wa kijasiriamali hawawezi kucheka na watu wanaokwepa kodi
kwa sababu kodi ndio uchumi. Mjasiriamali yeyote hupambana ili afikie
hatua na kujitegemea. Wanaofanyabiashara wanatambua kuwa kadiri
unavyokuwa na pesa yako binafsi (owners equity) ndivyo unavyokuwa na
uhuru na nguvu. Tunataka Rais na wabunge ambao watapambana kufa na
kupona kuhakikisha kampuni tunayowapa (nchi) inafikia ama inaanza
kuelekea kwenye kujitegemea zaidi.
Kuwa na
wabunge ambao kutwa kucha wanapiga kelele kuhusu miradi iliyokwama
kutokana na ukosefu wa fedha; na wakati huohuo hawapo tayari kusamehe
posho zao; bado ni mzigo kwa nchi hii. Kiongozi anaesimama majukwaani
kusisitiza vijana wajiajiri halafu yeye mwenyewe hana hata mpango wa
walau kufuga mbuzi tu nyumbani kwake; huyo hawezi kushawishi vijana
kujiajiri.
Kwanza
vijana hawa wanaoambiwa wajiajiri huwa wanahisi kama wanachorwa tu, kwa
sababu viongozi wao hawana mkao wa kijasiriamali. Wanaoambiwa wajiajiri
kuna wakati hujiuliza, ikiwa kujiajiri ni kuzuri mbona hao wanaotambia
hawaachi ajira zao kuja kujiajii? Mbona kila siku wanahangaika
kuwapachika watoto na ndugu zao katika hizo ajira?
Ifahamike
kwamba sifa nyingine ya mjasiriamali ni kutokuwa na upendeleo. Katika
kila nafasi anazangatia uwezo na sio kujuana na kubebena. Ukiwa na duka,
kampuni ama biashara yeyote halafu linapokuja suala la wafanyakazi
ukawa unawaajiri ama kuwaweka kwa kufahamiana, kulindana na kubebana
pasipo kuzingatia uwezo; ninakuthibitishia kuwa hufiki mbali,
utafilisika.
Tunataka
Rais, wabunge na madiwani ambao wataichukulia nchi hii kama biashara
inayotakiwa kuzalisha faida. Kama zipo hasara zilizotokea huko nyuma
basi vitabu vifungwe, zipigwe hesabu mpya ili biashara hii iitwayo
Tanzania ianze kuzalisha faida.
Uti wa
mgongo wa ujasiriamali ni uaminifu na uadilifu. Ukikosa uaminifu na
uadilifu biashara ni lazima ikushinde. Wateja watakuchukia, wafanyakazi
watakuchukia na utaporomoka tu. Tunamsubiri Rais mjasiriamali, wabunge
wajasiriamali na madiwani wajasiriamali. Hawa ni wale ambao watakuwa na
rekodi za uaminifu na uadilifu na ambao wataendesha biashara yetu
iitwayo Tanzania katika misingi hiyo.
Ninatamani
nchi impate Rais, wabunge, madiwani na kisha mawaziri ambao wamebeba
roho na maono ya kijasiriamali mioyoni mwao(entrepreneural spirit and
visions). Rais ambae ataagiza kile kinachochukuliwa kwa uzito, mawaziri
ambao wataonesha matokeo yanayofanana na sera na madiwani ambao
watapanga wanachokielewa.
Nchi yetu
haina mkao wa kijasiriamali kabisa. Wenye kutunga sera na wenye
kusimamia ni kama wanaishi sayari tofauti. Sera inasema kuwawezesha
akina mama na vijana wajitegemee kivipato. Lakini mwanamama akianzisha
biashara ya mama Ntilie Mgambo sio tu wanamkataza kutafuta hicho kipato,
bali wananyang'anya kabisa na mtaji! Machinga akipanga vitu vyake FFU;
hawa hapa; kumpiga mabomu.
Huwezi
kuwalaumu mgambo ama FFU kwa sababu wanatumwa. Huwezi kuwalaumu
wanaowatuma kwa sababu hawajui walitendalo. Laiti wangejua maumivu
anayopata mjasiriamali pindi unapomfukuza mahali penye wateja ama
unaponyang'anya mtaji wake, wasingekuwa wanatenda wayatendayo.
Ujasiriamali ni roho na katika uchaguzi wa mwaka huu natamani tuwapate
viongozi wenye roho ya ujasiriamali.
Sifa
nyingine ya mjasiriamali ni kuishi kwa alichonacho(living within your
means). Tunataka viongozi ambao kwa dhati kabisa watatuita wananchi na
kutuambia Jamani enhee, tulichonacho ni hiki na tunagawana kidogo
kidogo.Kama hakuna wanaokomba mboga, wananchi tutaelewa tu, maana chako
kidogo kina heshima kuliko kingi chenye masimango.
Mimi
hainisumbui, Rais, wabunge na madiwani watatoka chama gani,
ninachokizingatia ni mtazamo wao(mindset) katika eneo hili la
ujasiriamali. Iwe ni kutoka UKAWA ama CCM, iwe ni kutoka mgombea binafsi
ama vyama vingine vya upinzani; kura yangu nitampa kiongozi mwenye roho
na maono ya kijasiriamali.
Ninachofurahi
na kuamini ni kwamba chama changu cha siasa (maana mimi ni mwanachama
wa kawaida katika chama changu) kitazichanga vema karata zake na
kutuletea wagombea wanaouzika kwa muktadha huu wa roho ya kijasiriamali.
Tanzania inahitaji viongozi wajasiriamali
stepwiseexpert@gmail.com, 0719 127 901
No comments:
Post a Comment