Katibu
Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Alphayo Kidata
(kulia) bakitoa tathmini ya zoezi la bomoa bomoa awamu ya tatu
linaloendelea katika Manispaa ya Kinondoni jana jijini la Dar es
salaam.Kulia ni Muhandisi wa Manispaa ya Kinondoni Baraka Mkuya. Baadhi ya
waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali wakimsikiliza Katibu Mkuu
wa Wizara ya Ardhi Bw. Alphayo Kidata (hayupo pichani) alipokuwa akitoa
tathmini ya zoezi la bomoa bomoa kwa wananchi waliovamia maeneo
yanayomilikiwa kisheria na watu wengine katika manispaa ya Kinondoni
jana jijini Dar es salaam.
Baadhi
ya wananchi katika manispaa ya Kinondoni wakiondoa bidhaa zo katika
maduka eneo la Tegeta Machakani kupisha zoezi la bomoa bomoa kufuatia
maduka hayo kujengwa eneo lisiloruhusiwa, jana jijini Dar es salaam.
Moja ya ukuta uliojengwa kinyume cha sheria katika eneo lisiloruhusiwa eneo la Tegeta ukibomolewa jana.
Moja ya ukuta uliojengwa kinyume cha sheria katika eneo lisiloruhusiwa eneo la Tegeta ukibomolewa jana.
……………………………………………………………
Na. Aron Msigwa –MAELEZO, Dar es salaam.
Dar es salaam.
Wizara ya Ardhi, Nyumba na
Maendeleo ya Makazi imesema kuwa itaendelea na zoezi la kuvunja nyumba
zilizojengwa katika maeneo ya wazi na yale yaliyochukuliwa kwa nguvu
kinyume cha sheria kutoka kwa wananchi wanaoyamiliki kihalali katika
maeneo mbalimbali nchini.
Kauli hiyo ilitolewa jana jijini
Dar es salaam na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. Alphayo Kidata
alipokuwa akitoa tathmini ya zoezi la bomoa bomoa awamu ya tatu linaloendelea katika Manispaa ya Kinondoni jijini la Dar es salaam.
Alisema kuwa wizara imekuwa
ikipokea malalamiko mengi kutoka kwa wananchi ambao maeneo yao
yamevamiwa na watu wengine kinyume cha sheria ambayo wao wanayoyamiliki
kihalali.
Alieleza kuwa kutumia kanuni
na taratibu zinazosimamia umiliki na matumizi ya ardhi nchini wizara
hiyo itaendelea kuchukua hatua na kuyabaini maeneo yote yenye migogoro
inayosababishwa na baadhi ya wananchi wasio na nyaraka halali za
umiliki kisheria kuingia kwenye viwanja vya wananchi.
“Sisi kama wizara tumekubaliana
kuwa zoezi hili litakuwa endelevu, wale wote waliovamia maeneo ambayo
sio yao yakiwemo maeneo ya wajane na kujenga majengo yao Serikali
itayabomoa kwa nguvu hata kama wamejenga maghorofa na Hoteli”
Amesisitiza.
Alisema kwa muda mrefu pamekuwa
na wimbi kubwa la migogoro ya ardhi inayosababishwa na tabia ya wananchi
wasio na nyaraka kisheria kuingia kwenye viwanja vya watu wengine wenye
hati za kumiliki ardhi kihalali na kuviendeleza kiuvamizi pasipokuwa na
vibali vyovyote vya ujenzi.
Bw. Kidata alibainisha kuwa
vitendo wanavyofanya wananchi hao ni kosa la jinai na kinyume cha
sheria ya ardhi namba 4 ya mwaka 1999 kifungu namba 175(1) kinachozuia
mwananchi yeyote kuingia na kuendeleza kwenye ardhi asiyoimiliki
kisheria.
Alisisitiza kuwa hakuna raia yeyote wa Tanzania
aliye juu ya sheria hivyo watanzania bila kujali hali walizo nazo wanao
wajibu wa kutii na kufuata sheria za nchi zinazosimamia sekta ya ardhi
na kuongeza kuwa Serikali haitamvumilia yeyote atakayeendesha vitendo
vya kuhujumu maeneo ya wazi, kujenga kuta katika maeneo yasiyoruhusiwa
na kuvamia maeneo ya hidhadhi ya Bahari.
Kwa upande wake Muhandisi wa
Manispaa ya Kinondoni, Baraka Mkuya ambaye zoezi hilo lilifanyika katika
manispaa anayoisimamia ameeleza kuwa awamu ya tatu ya zoezi la bomoa
bomoa katika manispaa hiyo limehusisha ubomoaji wa kuta, majengo na
maduka katika maeneo ya tofauti ya kata Mikocheni B na Tegeta.
Aliongeza Wizara ya Ardhi,
Nyumba na Maenedeleo kwa kushirikiana na manispaa ya Kinondoni na vyombo
vya ulinzi na usalama itaendelea na zoezi hilo ili kusimamia sheria za
nchi kutokana na baadhi ya wananchi kwa makusudi kuendesha vitendo vya
hujuma na vurugu miongoni mwa jamii.
“Kwa upande wetu kama manispaa
ya Kinondoni kwa kushirikiana na Wizara na vyombo vya ulinzi na usalama,
tutalifanya zoezi hili kuwa endelevu ili tuweze kuondoa kabisa migogoro
ya ardhi katika manispaa yetu” Alisisitiza.
No comments:
Post a Comment